Thursday 30 January 2014

Man city yashikilia usukani England

Mshambulizi Sergio Aguero wa Man City

Klabu ya Manchester City imechupa hadi kileleni mwa ligi kuu ya soka nchini England baana ya kuonesha soka safi dhidi ya klabu ya Tottenham katika uga wa White Hart Lane.

Kikosi cha kocha Manuel Pellegrini kilihitaji ushindi dhidi ya Spurs ili kuwapiku Arsenal kwenye jedwali la msimamo wa ligi hiyo, na matumaini hayo yalianza kuonekana mapema wakati Aguero alipovuna bao la kwanza, hii ikiwa ni mara ya nane mfululizo akiifungia City katika mechi nane mfululizo.

Yaya Toure aliiweka Man City kifua mbele kwa bao la pili, dakika ya tano kipindi cha pili kupitia mkwaju wa penalti uliozua utata ambapo mlinda ngome wa Spurs Danny Rose alitimuliwa uwanja kwa kulishwa kadi nyekundu japo alionekana kuugusa mpira kwanza kabla ya kuadhibiwa kwa kumchezea rafu Edin Dzeko.

Dzeko aliongeza bao la tatu na ingawa Etienne Capoue alifunga bao la kufuta machozi kwa Spurs, bado kulikuwa na fursa kubwa kwa Man City kuendelea kuinyeshea Spurs mvua ya magoli kupitia mchezaji wa akiba Stevan Jovetic aliyefunga bao lake la kwanza katika ligi kuu tangu uhamisho wake wa pauni £22m kutoka klabu ya Fiorentina ya Italia.

Aguero afunga mabao 50

Baada ya mechi hiyo Sergio Aguero sasa ameandikisha rekodi ya kufunga takriban mabao 50 ya ligi kuu baada ya mechi 81, na kuibuka kuwa mtu wa tano kufunga kiasi hicho cha mabao, baada ya Andy Cole, Alan Shearer, Ruud van Nistelrooy na Fernando Torres.

Kisha City ikaongeza maumivu zaidi kwa Spurs baada ya kile kipigo cha mabao 6-0 mwezi November mwaka uliopita, pale Vincent Kompany alipokamilisha kibarua kwa kufunga bao la tano na la ushindi.

Chelsea 0 - 0 West Ham

Kwenye matokeo ya mechi nyinginezo Chelsea ilipata pigo kwenye harakati zake za kutafuta uongozi kwenye jedwali baada ya kulazimika kutoka sare ya kutofungana na West Ham katika uwanja wa nyumbani Stamford Bridge.
Kwingineko Aston Villa iliishinda West Brom mabao 4 - 3 nayo Sunderland ikainyuka Stoke 1-0.

Hii ndiyo orodha ya saba bora tarehe 30-01-2014:

1 Man City 53
2 Arsenal 52
3 Chelsea 50
4 Liverpool 46
5 Tottenham 43
6 Everton 42
7 Man Utd 40

No comments: