Friday 17 January 2014

Tanzania nimeona straika mmoja tu


MUINGEREZA Stewart Hall ametamka kuwa, straika wa Azam FC, Muivory Coast, Kipre Tchetche anaweza kucheza soka mahali popote katika klabu yoyote Ulaya na huwezi kumfananisha na mchezaji mwingine Tanzania.

Hall, kocha wa zamani wa Azam lakini sasa yuko nchini chini ya klabu ya Sunderland ambayo ina kituo cha soka kwa vijana cha Kidongo Chekundu, Dar es Salaam.

Akizungumza na Mwanaspoti, Hall alisema: “Nimekaa Tanzania najua uwezo wa wachezaji, Kipre ni mzuri anaweza kucheza mpira mahali popote na atafanikiwa. Tchetche ana akili, mwepesi kushika kitu chochote utakachomwelekeza, anajituma na wakati wote anataka kujua.”

“Mbali na hivyo, ana umbo zuri, nguvu, kasi, uhodari wa mashuti kiujumla ana kila sifa. Nimefundisha mpira nchi tofauti Ulaya na Afrika, naelewa uwezo wa Tchetche.”

Akaenda mbali zaidi kwa kusema kuwa sababu inayomfanya Tchetche asitoke nje kwenda kucheza kwenye mataifa makubwa ni maslahi anayopata Azam.

Mwanaspoti ilimtafuta Tchetche kueleza siri ya mafanikio yake naye alisema: “Ni kujituma na kufuata maelekezo ya mwalimu, lakini kujitambua pia.”

No comments: