Thursday 13 February 2014

Kizimbani kwa kumshambulia mtoto

Mkazi mmoja wa Kitangiri jijini Mwanza, Sophia Rafael (32), amepandishwa kizimbani kwa tuhuma za kumng’ata kidole mtoto wake.

Wakili wa Serikali, Juma Sarige, alidai mbele ya Hakimu wa Wilaya ya Nyamagana, Janeth Masesa, kuwa mshtakiwa alitenda kosa hilo Februari 9 mwaka huu.

Alidai kuwa siku ya tukio, mshtakiwa alimng’ata kidole mtoto wake wa umri wa miaka 10, akimtuhumu kumwibia Sh5,000.

Upande wake mtoto huyo alidai kuwa mama yake alimfanyia kitendo hicho na kusababisha kidole kukatika.

Upande wa jirani aliyejitambulisha mbele ya mahakama hiyo kuwa Jenifa Mbando (30), alidai kuwa aliposikia sauti ya mtoto huyo akipiga kelele alitoka nje na kutaka kujua kipi kilichokuwa kinaendelea.

Alisema baada ya muda mfupi, alimwona mtoto huyo akitokwa na damu nyingi mkononi na kwamba alichukua uamuzi wa kumpeleka hospitalini.

Hata hivyo mama huyo alidai kuwa hakufanya kwa makusudi ila alizidiwa na hasira.

Hakimu Masesa aliahirisha kesi hiyo hadi Februari 5 mwaka huu itakapotajwa tena.

No comments: