Friday 7 February 2014

Mtuhumiwa auwa askari kwa kumpiga jiwe

Askari polisi F. 5264 PC Sabato (37) wa Kituo cha Polisi cha Longido, wilayani Monduli, ameuawa kwa kupigwa jiwe na mtuhumiwa aliyekuwa akimpeleka mahabusu katika Gereza la Kisongo.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alisema mauaji hayo yamefanywa na mtuhumiwa aliyekuwa akipelekwa mahabusu baada ya kukosa dhamana katika kesi ya kuvunja na kuiba.

Kwa mujibu wa kamanda huyo, kesi hiyo iko katika Mahakama ya Wilaya ya Longido.

“Baada ya kufika njia panda ya Gereza la Kisongo, mtuhumiwa alimwomba PC Sabato amfungue mkono ili ajisaidie haja ndogo, lakini alipofunguliwa, ghafla aliokota jiwe na kumpiga askari huyo kwenye paji la uso, akaanguka na kuzimia,” alisema Kamanda Sabas

Kamanda Sabas alisema kwa mujibu wa waendesha bodaboda walioshuhudia tukio hilo, baada ya askari kuanguka chini, mtuhumiwa alitumia pingu aliyokuwa amefungwa mkononi, kuendelea kumshambulia kabla ya kutimua mbio.

Alisema hata hivyo waendesha bodaboda waliamua kumkimbiza na kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa.

Kamanda huyo alisema kitendo hicho kilifuatiwa na kutoa taarifa katika Kituo Kidogo cha Polisi cha Uwanja wa Ndege na baada ya muda, askari walifika na kumchukua pamoja na majeruhi ambaye hata hivyo, alifariki dunia usiku wa kuamkia jana, katika Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru.

Kwa mujibu wa Sabas, polisi wanaendelea kumhoji mtuhumiwa kabla ya kupandishwa kizimbani kwa shtaka la mauaji.

No comments: