Saturday 26 April 2014

Samatta apiga ‘ hat trick’ TP Mazembe

straika wa TP Mazembe, Mbwana Samatta akiokota mpira kwenye nyavu za timu pinzani

 
NYOTA ya straika wa Mbwana Samatta imezidi kung’aa klabuni TP Mazembe baada ya juzi Jumatano kuifungia mabao matatu ‘Hat Trick’ timu yake na kuisaidia kushinda mabao 4-1 dhidi ya AS Vita.
Katika pambano hilo la watani wa jadi kuwania ubingwa wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) lililochezwa kwenye Uwanja wa Stade TP Mazembe huko Kamalondo, Lubumbashi, Mtanzania huyo alionekana kuwa mwiba mkali kwa AS Vita yenye makao makuu yake Kinshasa.
Samatta aliyekuwa anaichezea Simba kabla ya kujiunga na TP Mazembe, alifunga mabao hayo katika dakika za 51, 71 na 85 huku Rainford Kalaba akiwa wa kwanza kuifungia timu hiyo katika dakika ya nane. Bao la AS Vita lilifungwa na Patou Ebunga dakika ya 16.
Tangu alipojiunga na TP Mazembe mwaka 2011, Samatta amekuwa mmoja kati ya wachezaji tegemeo wa timu hiyo kiasi cha kujizolea mashabiki wengi katika kila pembe ya Lubumbashi na kuipeperusha vizuri Bendera ya Tanzania.
Samatta sambamba na Mtanzania mwingine anayechezea timu hiyo, Thomas Ulimwengu waliitwa katika kikosi cha Taifa Stars kitakachocheza mechi ya kirafiki na Burundi kesho Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, lakini wameshindwa kuja kutokana na majukumu yao katika klabu hiyo.
Keshokutwa Jumapili, Samatta anatarajiwa kuichezea tena TP Mazembe dhidi ya Don Bosco katika mwendelezo wa michuano hiyo.

No comments: