Saturday 26 April 2014

Tambwe ahamishia nguvu ufukweni

LIGI Kuu Bara msimu wa 2013/14 imemalizika huku straika wa Simba, Amissi Tambwe, akiibuka Mfungaji Bora baada ya kufunga mabao 19. Lakini mchezaji huyo amekaa siku chache tu nje ya uwanja na sasa anafanya mazoezi katika ufukwe wa Coco jijini Dar es Salaam.
Akiwa ufukweni hapo, Tambwe hufanya mazoezi ya kukimbia ili kuongeza pumzi za kupambana uwanjani na yale ya kujenga stamina ili aweze kuwapenya kwa nguvu mabeki wa timu pinzani.
Yote hayo anajiandaa kwa msimu mpya unaotarajiwa kuanza Agosti. Kwa mabao hayo 19 aliyofunga, Tambwe alimzidi straika wa Azam FC, Kipre Tchetche aliyefunga mabao 14 huku Didier Kavumbagu wa Yanga na Elius Maguli wa Ruvu Shooting,
kila mmoja akifanya hivyo mara 13. Akizungumza na Mwanaspoti, Tambwe ambaye alitarajiwa kuungana na kikosi cha Burundi kilichotarajiwa kuwasili jana jijini Dar es Salaam tayari kwa mechi ya kirafiki dhidi ya Taifa Stars ya kesho Jumamosi, alisema ameamua kufanya mazoezi ufukweni ili kujiweka vizuri kwa msimu ujao wa ligi.
Mechi hiyo itakayochezwa Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam pia ni sehemu ya maadhimisho ya sherehe za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
“Kwa sababu kwa sasa mazoezi ya timu yamesimama kwa muda, huwa naenda kwenye fukwe wa Coco na kufanya mazoezi yangu binafsi kama kukimbia na mambo mengine,” alisema.
“Huwa sifanyi kila siku, ila sina siku maalumu, inategemea na siku hiyo nahitaji kufanya mazoezi yangu kwa namna gani.
“Hii yote nafanya kwa sababu maisha yangu yanategemea soka hivyo lazima nihakikishe nipo vizuri muda wote ili mambo yasiniharibikie, si unajua mpira sasa ni ushindani? Hakuna anayekubali kuachwa kirahisi uwanjani.”
Tambwe ni miongoni mwa wachezaji wa kigeni walioonyesha uwezo mkubwa katika kuzifumania nyavu na kuongeza msisimko wa ligi kuu, raia wa kigeni wengine waliofanya vizuri katika ligi hiyo ni Tchetche raia wa Ivory Coast, Mrundi Kavumbagu wa Yanga na Mganda Hamis Kiiza pia wa Yanga aliyefunga mabao 12.
Tambwe alijiunga na Simba mwanzoni mwa msimu uliopita akitokea Vital’O ya Burundi sambamba na beki Gilbert Kaze. Hata hivyo Kaze hakucheza mechi za mzunguko wa pili kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya goti.

No comments: