Monday 14 April 2014

TBC ya vuruga mchakato mzima wa bunge la katiba

Dodoma. Shirika la Utangazaji Nchini (TBC) jana limevuruga mwenendo wa Bunge la Katiba baada ya kukata matangazo yake wakati mjumbe wa Bunge la Katiba, Tundu Lissu alipotoa ufafanuzi wa maoni ya walio wachache.

Mgogoro huo ulitokea bungeni jana wakati Tundu Lissu akitoa ufafanuzi kuhusu maoni ya wajumbe walio wachache wa kamati namba nne.

Wakati Lissu akiendelea na ufafanuzi huo, baadhi ya wajumbe walianza kunong’ona kuwa TBC imesitisha matangazo.

Hata hivyo, kauli hiyo ilimfanya Lissu kudharau na kuendelea na ufafanuzi wake.

Baada ya muda mfupi alisimama mjumbe wa Bunge hilo, Freeman Mbowe na kuomba mwongozo kwa Mwenyekiti wa Bunge hilo kuhusiana na tukio hilo.

“Mjadala huu ni muhimu sana na mjadala huu umekuwa ukirushwa na kituo cha televisheni cha Taifa TBC muda wote tangu tumeanza. Hivi punde kuna taarifa kuwa TBC wamekata matangazo yote ya Redio na Televisheni una nini cha kuwaeleza Watanzania?”alihoji Mbowe.

Akijibu mwongozo huo, Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta, alisema taarifa ya TBC kufunga matangazo ni ya kushtua sana kwa sababu Bunge Maalumu lina mkataba na serikali pamoja na TBC One wa kuhakikisha mjadala na matangazo yote ya Bunge hilo yanaonekana na kuwafikia wananchi.

“Naomba Katibu achunguze mara moja, aangalie nini kimetokea kama ni tatizo la muda ama la kiufundi na tutapata majibu sasa hivi,”alisema na kulazimu Bunge hilo kusimama kwa muda.

Baada muda mfupi, Sitta alisema tatizo ni hali ya hewa jijini Dar es Salaam.

“Katibu amepanda huko juu katika studio na maelezo ya kitaalamu yanasema hali ya hewa Dar es Salaam,” alisema kauli iliyoamsha kelele kutoka kwa baadhi ya wajumbe hao huku wengine wakisikika wakisema barabara zimekatika na uwanja wa ndege umefungwa jana.

Hali hiyo ilimbidi Sitta kuwasihi wajumbe hao kutulia kwa sababu mambo yote yangetengezwa.

“Ni hivi kwa sababu yoyote ile hatuwezi kuendelea,” Hali hiyo iliibua nderemo na vifijo kutoka kwa baadhi ya wajumbe huku wakitamka “Sitta, Sitta, Sitta.”
“Natoa maelekezo kwa Katibu wa Bunge kuangalia muda ambao matangazo yalizimika wakati Lissu akiongea ili Jumatatu tutakaporejea nimpe nafasi ya kwanza ya kumalizia ule muda wake,”alisema huku mjumbe wa Bunge hilo, Dk. Khamis Kigwangallah ambaye awali alisoma taarifa ya kamati hiyo, akipaza sauti kuomba mwongozo.

Alipopewa nafasi Kigwangallah, alihoji iwapo ufafanuzi wa wachache unaweza kuahirishwa kwasababu kituo cha televisheni hakionyeshi.

Akijibu mwongozo huo, Sitta alisema,” Jambo tunalolifanya ni kubwa sana. Tumeweka bajeti maalumu na warusha matangazo wakawekwa hapa kwenye studio kufanya kazi hiyo maana yake ni kuwashirikisha wananchi wanaofuatilia kwa hamu Bunge hili.”

No comments: