Thursday 22 May 2014

Rais Banda Adai uchaguzi umekumbwa na udanganyifu


Rais Banda
Uchaguzi wa Malawi ulikumbwa na visa vingi vya wizi wa kura pamoja na udukuzi wa mitambo iliyokuwa inatumiwa kujumlisha kura. Haya ni madai ya Rais Joyce Banda.
Rais Joyce Banda ametaka kura hizo kuhesabiwa upya bila ya kutumia mitambo ya elektroniki ya kuhesabu kura.
Bi Banda alikumbwa na ushindani mkali katika uchaguzi huo uliofanyika siku ya Jumanne kutoka kwa wagombea watatu akiwemo, waziri wa zamani wa mambo ya nje Peter Mutharika.
'Waziri ajiua'
Mapema Alhamisi naibu waziri wa serikali za mitaa wa Malawi alijipiga risasi na kujiua nyumbani kwake mjini Lilongwe.
Godfrey Kamanya alikuwa anagombea kutetea kiti chake cha ubunge katika jimbo la Nzonzi Kusini.
Shughuli ya kuhesabu Kura Malawi
Alijiua alfajiri ya leo katika mojawapo ya vyumba vya nyumba yake iliyopo Area Ten mjini Lilongwe.
Mwili wa marehemu umehifadhiwa kwenye hospitali kuu ya Kamuzu mjini humo, na jeshi la polisi litatoa taarifa rasmi ya kifo hicho baada kukamilisha uchunguzi.
Haijajulikana sababu za Kamanya kujiua japokuwa ameacha barua ya maelezo ambayo polisi wataitoa baadae.
Matokeo ya kura bado hayajatangazwa rasmi katika kile kinachosemekana kuwa uchaguzi wenye ushindani mkali sana.
Afisa mkuu wa uchaguzi, amesema kuwa mfumo wa elektroniki umeharibika na maafisa wanatumia matokeo kwa njia ya barua pepe.

No comments: