Wednesday 4 June 2014

Kongamano kuhusu nishati endelevu laanza New York

watu wa asili nchini Mongolia wakitumia mabamba ya nishati ya jua katika ger, hema lao la kiasili
Kongamano la siku tatu kuhusu nishati endelevu kwa wote limeanza leo hapa New York, kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa. Joshua Mmali na taarifa kamili
Taarifa ya JOSHUA
Kongamano hilo linawaleta pamoja wadau kutoka mashirika mseto ya ubia, likilenga kuongeza kasi ya uchukuaji hatua katika sekta ya biashara na serikalini, kuchagiza ushiriki wa mashirika ya umma na vijana, pamoja na kuongeza upatikanaji wa nishati endelevu kwa kuwawezesha wanawake.
Washiriki kwenye kongamano hilo pia wanaangazia masuala ya kuchagiza uwekezaji katika nishati endelevu kupitia mifumo bunifu ya biashara, na kwa kubadilishana ujuzi na uzoefu. Mmoja wa washiriki ni Mariam Mohamed Abdallah, wa shirika la Youth Climate Movement
Sauti ya Mariam
"Uendelevu unahusu elimu, upatikanaji wa rasilmali, na kadhalika, lakini tunapozungumzia umaskini na utulivu, tunaangalia umaskini wa nishati. Ni lazima tuutokomeze umaskini wa nishati, kwa njia endelevu, kwa sababu umaskini wa nishati na umaskini wa rasilmali kwa ujumla, huchangia migogoro na kutishia utulivu, na hivyo kuharibu mazingira ya maendeleo na uendelevu."
Hapo kesho, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anatarajiwa kulihutubia kongamano hilo, ambapo pia atazindua rasmi Mwongo wa Umoja wa Mataifa wa Nishati Endelevu kwa Wote

No comments: