Thursday 12 June 2014

Majambazi wavamia kituo cha polisi na kufanya mauaji Dar

Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Polisi, Paul Chagonja

Hili linawezekana kuwa ni tukio la kwanza na la aina yake. Majambazi wanaokisiwa kuwa sita, wakiwa na pikipiki tatu, juzi walivamia Kituo Kidogo cha Polisi Mkamba kilichopo Kimanzichana, Wilaya ya Mkuranga, Pwani na kuua askari mmoja na mgambo na kujeruhi mgambo mwingine na kisha kupora bunduki tano na risasi 60 usiku wa kuamkia juzi.
Polisi aliyeuawa ni Konstebo Joseph Ngonyani na majeruhi Venance Francis na Mariamu Mkamba ambao walipelekwa katika Hospitali ya Wilaya Mkuranga kwa matibabu.
Kwa mujibu wa wakazi wa eneo hilo, majambazi hayo yalikuwa na taarifa kwamba kituo hicho kina silaha za moto na kuweka mpango wa kukivamia usiku baada ya kupiga hesabu na kujiridhisha kwamba polisi kutoka Kibiti, wilayani Rufiji au Mkuranga wasingeweza kufika hapo kabla ya wao kutekeleza azma yao.
Mkazi wa Kimanzichana, Mohamedi Muba alisema wananchi wenzake walimwambia kuwa majambazi hayo yalifika kituoni hapo saa saba usiku na kuvamia kituo hicho wakitaka funguo za kufungulia stoo zilipohifadhiwa silaha.
“Kituo cha Kimanzichana kipo mbali sana na vituo vingine vya Kibiti na Mkuranga, ni kama kilometa 30 hadi 35, hivyo kwa wakati huo wa usiku wa manane ingekuwa vigumu kuwahi kutoa msaada,” alisema mkazi mwingine ambaye hakutaka kutajwa jina.
Mkazi huyo alisema baada ya kubishana na askari huyo aliyekuwa na ufunguo, majambazi hayo yalitumia nguvu kumlazimisha kutoa funguo.
Huku mzozo huo ukiendelea, majambazi wengine walikuwa wakiwashambulia askari mgambo kwa mapanga na walipoona askari amegoma kutoa funguo walimpiga risasi na kuzichukua kisha kufungua na kuchukua silaha na kutokomea kusikojulikana.
Alisema majambazi hayo yalionekana kujipanga na kuwa na taarifa zote kuhusu hali ya ulinzi katika kituo hicho.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Ulrich Matei alipoulizwa kuhusiana na tukio hilo, alisema ameagizwa na Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Polisi, Paul Chagonja kwamba ndiye atakayelizungumzia suala hilo.
“Kwa sasa nipo chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ninashughulikia mwili wa askari aliyeuawa, Makao Makuu watalizungumzia zaidi,” alisema Kamanda Matei.
Chagonja alonga
Akizungumzia tukio hilo jana, Chagonja alisema majambazi hayo yalitumia bunduki na mapanga kumuua askari huyo na kuwajeruhi mgambo hao na kutokomea na bunduki mbili aina ya Sub Mashine Gun (SMG), mali ya Jeshi la Polisi na bunduki tatu aina ya shortgun, mali ya raia ambazo zilikuwa kituoni hapo zikisubiri kupelekwa kwenye ghala kuu la silaha.
“Polisi inalaani vikali kitendo hicho na imeanzisha msako mkali na itahakikisha inayatia mbaroni majambazi hayo,” alisema Chagonja.
Aliwaomba wananchi wenye taarifa za wahalifu hao kujitokeza au kupiga simu ili waweze kuyakamata na kuyafikisha mahakamani na kupata silaha hizo. Alitoa namba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania (IGP), Ernest Mangu na ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani ambazo ni 0754 785 557 na 0715 009 953 kwa ajili ya kutoa taarifa zitakazowezesha kupatikana kwa watu wenye silaha au wanaotiliwa shaka kuhusiana na tukio hilo.
“Kwa sasa wananchi wawe watulivu, waendelee na shughuli zao lakini wafahamu muda wote polisi hatutalala, tutayasaka usiku na mchana na tutahakikisha tunayatia mbaroni,” alisema.
Kimanzichana na Mkuranga
Habari za majambazi hayo kuvamia kituo hicho zilisambaa haraka mapema asubuhi kutokana na msako mkali ulioanza kufanywa muda mfupi baada ya tukio hilo.
Madereva wanaotumia barabara ya Dar es Salaam - Kilwa walisema magari yote yalisimamishwa katika vizuizi na kupekuliwa.
“Kila gari lililopita katika Kijiji cha Kimanzichana lilifanyiwa upekuzi ili kutafuta silaha hizo, ukikutwa na mkaa au mbao kazi unayo,” alisema dereva wa daladala, Hussein Ali.
Alisema kutokana na msako huo, madereva wengi walisitisha safari na dereva mmoja alisikika akimweleza mwenzake aliyekuwa akielekea huko... “Usiende Mkuranga leo kuna msako mkali, usipokutwa na mkaa au mbao gari lako hata likiwa na tatizo dogo tu utakamatwa.”

No comments: