Sunday 22 June 2014

Nigeria waichapa Bosnia-Hercegovina 1 -0

Emenike alichangia pakubwa mechi hii
Nigeria ilisajilia ushindi wake wa kwanza katika kombe la dunia katika kipindi cha miaka 16 ilipoilaza Bosnia-Hercegovina 1-0 katika mechi yao ya pili ya kundi F.
Ushindi wa mwisho wa Super Eagles ilikuwa ni mwaka wa 1998.
Bao hilo la pekee lilifungwa na Peter Odemwinge kunako dakika 29 ya kipindi cha kwanza alipopokea pasi safi kutoka kwa Emenike .
Mfungaji bao hilo Peter Odemwinge naye alifunga bao lake la kwanza la kombe la dunia baada ya miaka minne.
Bao hilo hata hivyo litajadiliwa kwa upana na marefu ikizingatiwa kuwa wachezaji wa Bosnia walimlalamikia vikali refarii wa mech hiyo wakisema kuwa Emenike alikuwa ameponda nahodha wa Bosnia Spahic kabla ya kummegea odemwinge pasi murwa.
Odemwinge akiifungia Nigeria bao dhidi ya Bos- Hez
Aidha msaidizi wa refarii atakumbukwa kwa kumnyima bao safi Edin Dzeko aliyesemekana kaotea lakini picha za runinga zilionesha haikuwa kweli na hivyo Bosnia watelekea nyumbani wakijua vyema kuwa mechi hiyo ingeishia sare ya Moja kwa moja isingalikuwa ni msaidizi wa refarii.
Kipa wa Super Eagles Vincent Enyeama alikuwa na wakati mgumu kumzima Dzeko aliyefanya mashambulizi katika muda wa majeruhi katika mechi hii.
Nigeria sasa itakabiliana na Argentina katika mechi yao ya mwisho ya makundi .
Kufuatia Ushindi huo Super Eagles imejikita katika nafasi ya pili ikiwa na alama 4 mbili nyuma ya vinara Argentina ambao walilazimika kufanya kazi ya ziada kuilaza Iran bao 1-0.
Iran ni ya tatu huku Bosnia ikiyaaga mashindano haya baada ya mechi yao ya mwisho dhidi ya Iran.
Nigeria itafuzu kwa mkondo ujao iwapo itashinda ama kutoka sare na Argentina katika mechi yao ya mwisho.
Vilevile Super Eagles itafuzu iwapo Bosnia itailaza Iran.

No comments: