Sunday 1 June 2014

UKAWA waipuuza CCM

Kiongozi wa UKAWA na Mjumbe wa Baraza Kuu la NCCR-Mageuzi, Juju DandaUMOJA wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) umewataka Watanzania kupuuza kauli za viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwakuwa hazina lengo la kuwasaidia katika mchakato wa uundwaji wa katiba mpya.
Mmoja wa viongozi wa UKAWA na Mjumbe wa Baraza Kuu la NCCR-Mageuzi, Juju Danda, alisema kauli za viongozi wa CCM zinalenga kutetea masilahi ya chama chao kinachotaka muundo wa serikali mbili tofauti na mapendekezo ya rasimu ya katiba inayotaka serikali tatu.
Alisema kuwa viongozi wa UKAWA wanasikitishwa na hujuma wanayofanyiwa wananchi ambapo CCM imepuuza mawazo yao waliyoyatoa kwa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Juju, alisema makada wa CCM hivi sasa wamekosa sera na wameanza propaganda za kudai kuwa wabunge wa vyama vya upinzani wamekuwa wakimtukana Mwalimu Julius Nyerere ilhali wakitambua kinachofanywa na upinzani ni kuhoji makosa yaliyofanyika miaka ya nyuma.
“Nawashangaa zaidi viongozi wa CCM ambao wanafikiri kukosolewa kwa viongozi walioasisi taifa hili ni kuwakashifu… wakumbuke kuwa kizazi cha sasa ni cha kuhoji zaidi,” alisema.

No comments: