Thursday 10 July 2014

Israel yaendeleza mashambulizi Gaza

 
Zaidi ya watu sabini wameuawa Palestina tangu mzozo kuanza kati ya Israel na Palestina

Ndege za Israel zimesababisha vifo vya wapalestina 9 waliokuwa wakitizama mchuano wa kombe la Dunia, ndani ya mgahawa mmoja katika mji wa Khan Yunis huko Gaza.
Jumla ya watu 20 wameuawa katika mashambulizi yaliyofanywa na Israel dhidi ya wapalestina katika ukanda wa Gaza usiku kucha.
Taarifa hii ni kwa mujibu wa maafisa wakuu wa kipalestina.
Wizara ya afya imesema kuwa wengi walifariki katika mashambulizi yaliyofanywa dhidi ya nyumba na mgahawa katika eneo la Khan Younis, Kusini mwa Palestina.
Vifo hivyo vimefikisha idadi ya watu waliofariki hadi 76 upande wa wapalestina tangu vita kuanza kati ya pande hizo mbili.
Wapiganaji katika ukanda wa Gaza waliendelea kurusha makombora nchini Israel Alhamisi usiku huku ving'oa vikisikika kila sehemu ya miji ya Kusini.
Msemaji wa wa Israeli awali alisema kuwa vifo vya watu 8 siku ya Jumanne ilikuwa ajali tu na haikuwa nia ya Isarel kusababisha vifo hivyo.
Israel bado haijatoa idadi ya watu wake waliofariki au kujeruhiwa lakini Palestina ingali inarusha makombora yake katika ardhi ya Israel.
Huku hayo yakijiri, Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa, Ban Ki-moon, ameonya kuwa hali huko Gaza imo ukingoni na huenda ikawa mbaya kiasi cha kutoweza kudhibitiwa.
Ban amesema eneo hilo haliwezi kuhimili vita vingine huku akitoa wito kwa pande zote zisitishe ghasia.
Amelitaka kundi la Hamas lisite kurusha makombora nchini Israel na ameiomba serikali ya Israel kujizuia na iheshimu jukumu lake la kimataifa ili kuwalinda raia.

No comments: