Wednesday 23 July 2014

Mabeki wa Chelsea walipomkaba mchezaji mnene zaidi duniani

JUMAMOSI jioni, John Terry aliwaongoza mabeki wa Chelsea kukabiliana na mchezaji mnene na mwenye nguvu zaidi duniani, Saheed Adebayo Akinfenwa ambaye umbo lake linaleta kichekesho kikubwa kwa mashabiki wa soka.
Chelsea ilishinda mabao 3-2 wakati huu ikijiandaa na michuano mbalimbali msimu ujao, lakini walilazimika kukabiliana na Akinfenwa ambaye alikuwa katika ubora wake.
Hadi wakati anatolewa uwanjani dakika ya 60, Chelsea ilikuwa imekufa 2-0 huku Akinfenwa akimuhenyesha Terry na wenzake. Hata hivyo baadaye walifunga mabao matatu ya haraka haraka yaliyobadili matokeo ya mechi wakati Akinfenwa akiwa nje ya uwanja.
Licha ya umbo lake kubwa, Akinfenwa aliyezaliwa jijini London Mei 10, 1982 anadaiwa kuwa na kilo 86 tu lakini ana uwezo wa kubeba uzito wa kilo 180 ambazo ni mara mbili na uzito wake.
Tayari Fifa wamempitisha kama mchezaji mwenye nguvu zaidi duniani huku wakimuingiza katika Video zao za michezo ya kompyuta huku umbo lake likionekana kuwa kivutio kwa mashabiki wengi duniani.
Mlinzi wa klabu ya Vale iliyo daraja la kwanza England ambaye alicheza timu moja na Akinfenwa Northampton, Dan Jones anaeleza kwamba ni kujisumbua tu kujaribu kutumia nguvu kumkaba mchezaji huyo.
“Soka lake halibadiliki tangu tulipokuwa Northampton. Anapenda kuuficha mpira miguuni na inajionyesha wazi kwamba hana mpango wa kukimbia nao. Anapenda kukaa na mpira mguuni huku akiwasukuma walinzi kwa nguvu zake.” Anasema Jones.
“Hauwezi kushindana naye kwa nguvu kwa sababu utaishia kumfanyia rafu au atakutupa tu. Inabidi utumie akili sana wakati wa kumkaba. Inabidi usitumie nguvu nyingi sana kumkaba.”
“Wakati mwingine akipata mpira tunamuachia tu na kuangalia anachotaka kufanya kwa sababu tunajua hawezi kukimbia, yeye huwa anaaangalia watu wanaofungua nafasi tu.” Anasema Jones.
Akinfenwa amedai kwamba hajawahi kucheza katika Ligi Kuu ya England kwa sababu makocha wamekuwa wakiliogopa umbo lake na kudhani kwamba atakuwa mzigo tu uwanjani kitu ambacho sio cha kweli.
“Nadhani naweza kutisha Ligi Kuu. Nadhani niko sawa na Didier Drogba tu. Sijacheza madaraja ya juu kwa sababu kuna mtazamo fulani wa jinsi ambavyo mwanasoka anapaswa kuwa na mimi sionekani kuwa hivyo,” anasema Akinfenwa.
“Sitaki kuonekana mjinga lakini nimefunga zaidi ya mabao 150 katika mechi 300. Waulize walinzi au makocha wa timu pinzani watakwambia jinsi nilivyo balaa.” Anasema staa huyo
“Ningependa kukutana na John Terry na kumuharibu. Ningependa kukutana na wachezaji kama Nemanja Vidic hili niwaonyeshe inakuaje unapokumbana na mtu kama mimi.” Alijigamba staa huyo mzaliwa wa Islington London.
Akinfenwa amekiri kwamba anapenda sana kula lakini hapendi kula vyakula vya kisasa na anapenda kula zaidi vyakula vya Kiafrika.
“Nakula sana, lakini sio McDonald au migahawa ya vyakula vya haraka haraka. Lakini nadhani inabidi nipewe hisa na migahawa ya Nandos kwa sababu nakula sana pale.”
Akinfenwa anavaa jezi kubwa (XXL) mara zote amekuwa akiandamwa na mashabiki wa timu pinzani ambao huwa wanaimba kuwa mchezaji huyo ana uwezo mkubwa wa kula nyama nyingi kuliko kufunga mabao mengi.
“NImekubali kwamba inabidi nikutane na mashambulizi haya. Nakubali kwamba nina umbo kubwa na ningesikitika kama nisingekuwa hivi. Mara nyingi nakumbana na haya na ninapokumbana nayo huwa nafunga.”
“Kitu kinachonifurahisha ni pale wanaposema kuwa mimi ni mnene kama Eddie Murphy. Napenda mashabiki wa timu pinzani wanaponishambulia kwa sababu mimi uwanjani naendelea kufunga tu.”
“Kama ningekuwa nasijikia kuwa mnene au mvivu, basi ningefanya kitu kupunguza unene wangu. Sijawahi kufanya mazoezi ya kupunguza uzito na makocha wengi walionifundisha wanakubaliana na ukweli kwamba umbo langu ndivyo lilivyo.”
Akinfenwa ni mmoja kati ya wachezaji waliocheza timu nyingi England. Mpaka sasa akiwa na umri wa miaka 32 licha ya kutocheza katika Ligi Kuu ya England lakini amecheza klabu 14 za madaraja ya chini.
Timu hizo ni FK Atlantas, Barry Town, Boston United, Leyton Orient, Rushden & Diamonds, Doncaster Rovers, Torquay United, Swansea City, Millwall, Northampton Town, Gillingham,Northampton Town, Gillingham na AFC Wimbledon.

No comments: