Monday 27 October 2014

Serikali ya Kana Tuhuma zinazo mkabili Nyalandu

SERIKALI imesema tuhuma zilizokuwa zikitolewa na baadhi ya vyombo vya habari dhidi ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, hazina ukweli na zimelenga kumchafua binafsi pamoja na wizara.
Pia imetoa ufananuzi wa tuhuma hizo zilizokuwa zikielekezwa kwa Nyalandu na kuonya kuwa, kuanzia sasa itachukua hatua kali za kisheria dhidi ya wanaomchafua na kupaka matope utendaji kazi wake.
Hivi karibuni Nyalandu amekuwa akiandamwa na baadhi ya watu kwa kile kinachodaiwa kuwa ni hatua yake ya kudhibiti mtandao hatari wa ujangili na kuziba mianya ya ulaji ndani na nje ya wizara hiyo.
Taarifa ya Wizara ya Maliasili na Utalii, iliyotolewa kwa vyombo vya habari jijini Dar es Salaam jana, ilisema tuhuma hizo zimelenga kuchafua utendaji kazi wa Nyalandu na watendaji wengine.
Ilisema baadhi ya vyombo hivyo vya habari (si Uhuru), vimekuwa vikichapisha habari ambazo hazina ukweli wala mashiko kwa jamii zaidi ya kuchochea chuki na uhasama.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, moja ya  habari hizo ni ile inayodaiwa kuwa Nyalandu ameuza hifadhi, kutoa leseni maalumu ya Rais kwa Familia ya Freidkin kwa ajili ya kuwinda idadi kubwa ya wanyama bure.
Taarifa hiyo ya wizara ilisema tuhuma hizo zimetolewa na watu wenye nia ovu na kumpunguzia dhamira, malengo na kasi ya kupambana na mtandao hatari wa ujangili nchini.
Ilisema Leseni ya Rais ya kuwinda kwa mujibu wa Kifungu cha 58 (1) cha Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009 ikisomwa kwa pamoja na Tangazo la Serikali Na. 273 la mwaka 1974, inampa mamlaka Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori baada kupata ridhaa ya Waziri mwenye dhamana ya wanyamapori kutoa kibali maalumu kwa malipo au bure.
Aidha, kibali hicho hutolewa baada ya Waziri kuridhika kwamba kina maslahi kwa taifa na hakikinzani na sheria na mikataba ya kimataifa kama CITES.
Kufuatana na Kifungu hicho cha 58 (1) Leseni Maalum hutolewa kwa mtu yeyote kwa masilahi ya taifa ikiwemo utafiti wa kisayansi, makumbusho, elimu na utamaduni au chakula wakati wa dharura.
Maslahi ya taifa ni pamoja na leseni kutolewa kwa watu mashuhuri kama vile wakuu wa nchi,  wafalme, malkia, wakuu wa dini na watu ambao katika utendaji wao wametoa michango yenye manufaa kitaifa au katika shughuli za uhifadhi wa wanyamapori.
Imewataja baadhi ya waliowahi kupewa leseni hiyo ya Rais kwa mwaka 2013 hadi sasa kuwa ni H.H. Sheikh Abdullah Mohamed Buli Al Hamed kupitia kampuni za Kilombero North Safaris/Green Mile Safaris, ambayo ilitolewa bure.
Nyingine ni H. H Sheikh Mohamed Rashid Al Maktoum kupitia kampuni ya Ortello Business Corporation (OBC), ambacho pia kimetolewa bure.
Familia ya Freidkin ya watu wanane kupitia kampuni ya Tanzania Game Trackers Safaris Ltd, ambacho kimelipiwa ada pamoja na Kiongozi wa Bohora Duniani, kilichotolewa bure.
Taarifa hiyo imesema kuwa, familia ya Freidkin imekuwa na sifa ya kupewa Leseni ya Rais kutokana na mchango wake mkubwa kwa taifa katika shughuli za uhifadhi wa Wanyamapori kwa kipindi cha zaidi ya miaka 20 iliyopita bila kukoma.
Imekuwa ikitoa mchango huo kupitia Kampuni ya Uwindaji wa Kitalii iitwayo Tanzania Game Trackers Safaris Ltd. Pamoja na Asasi yake iitwayo Freidkin Conservation Fund (FCF tangu miaka ya 1990).
FCF imekuwa ikitoa michango mikubwa hususan ya kukabiliana na ujangili pamoja na shughuli za kijamii.
Ilisema tuhuma ya kuwa Nyalandu amekiuka kifungu kinachoweka ukomo wa idadi ya vitalu ambavyo ni vitalu vitano kwa kampuni si za kweli.
Kwa kuzingatia maelezo hayo hapo juu, kutolewa kwa leseni ya Rais kwa familia ya Freidkin kulizingatia sheria, kanuni na taratibu zote za uwindaji.
Kuhusu tuhuma za Nyalandu kudaiwa kuuza hifadhi, taarifa hiyo ya serikali ilisema kuwa ni za uzushi na kuwa ukweli ni kwamba, waziri huyo alikwenda Afrika Kusini kwa kufuata taratibu rasmi na maagizo ya serikali kuhudhuria mkutano wa African Parks Network (APN) wa uhifadhi ulioandaliwa na asasi hiyo kwa lengo pia la kuhakiki uwepo, utendaji halisi wa taasisi hiyo na kufanya majadiliano kuhusiana na mapendekezo yao.
Imesema katika mkutano huo, hakukuwa na mikataba yoyote iliyowekwa na Nyalandu au maamuzi yoyote ya kukabidhi hifadhi za Taifa kama ilivyoelezwa katika baadhi ya vyombo vya habari husika.
Hata hivyo, taarifa hiyo imesema kuna mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kupambana na ujangili ikiwemo kupungua kwa kiasi kikubwa kwa mauaji ya tembo.

No comments: