Monday 17 November 2014

Msako mkali dhidi ya misikiti mjini Mombasa

 
Polisi nchini Kenya wamefanya msako mkali dhidi ya misikiti inayotoa mafunzo ya itikadi kali za kidini mjini Mombasa pwani ya Kenya.
Mtu mmoja ameuawa kwenye msako huo ulioanzishwa Jumapili dhidi ya misikiti inayosemekana kutoa mafunzo ya kuunga mkono harakati za kundi la wapiganaji wa kiisilamu la Al Shabaab nchini Somalia.
Misikiti ya kwanza kulengwa katika msako huo ni ile ya Masjid Musa na Sakina.
Viongozi kadhaa wa kiisilamu wameuawa mjini Mombasa hivi karibuni
Mkuu wa polisi mjini Mombasa alinukuliwa na shirika la habari la AFP akisema kuwa walipata taarifa kwamba kundi hilo limekuwa likipanga kufanya mashambulizi na hiyo ndiyo sababu ya msako huo kuanzishwa.
Watu 200 wamekamatwa ikiwemo washukiwa wakuu sita.
Polisi wanasema kuwa mtu mmoja aliuawa ingawa hawajatoa taarifa zaidi kuhusu kifo cha mtu huyo na kwamba uchunguzi utafanywa.
Viongozi kadhaa wa kidini wameuawa mjini Mombasa katika kinachodaiwa kuwa mauaji ya kiholela huku kukiwa na ushindani pamoja na uhasama kati ya makundi kinzani ya kiisilamu.
Makanisa pia yamekuwa yakilengwa kwa mashambulizi.

No comments: