Sunday 2 November 2014

Simba saba wauwawa kwa kuwekewa Sumu Serengeti

Kamanda wa Polisi wa Wilaya ya Serengeti, mkoani Mara, Pius Mboko na wahifadhi wa wanyamapori,wakimfanyia uchunguzi simba mmoja kati ya saba waliouawa juzi kwa kuwekewa sumu katika nyama baada ya kudaiwa kula ng’ombe wa mwanakijiji anayeishi kando ya Hifadhi ya Jamii ya Ikona.
Simba saba wamekutwa wamekufa Hifadhi ya Jamii ya Ikona (WMA) wilayani Serengeti, mkoani Mara baada ya mfugaji mmoja wa Kijiji cha Park Nyigoti kudaiwa kuwatega kwa sumu, kufuatia ng’ombe wake mmoja kukamatwa malishoni ndani ya hifadhi hiyo.

Tukio hilo lilibainika juzi ndani ya hifadhi hiyo Kijiji cha Park Nyigoti, baada ya mfugaji huyo Manyeresa Nguhecha akiongozana na askari wa Pori la Akiba la Ikorongo na walinzi wa Kampuni ya Grumeti Reserves na kukuta mizoga hiyo wakati akifuatilia eneo ambako ng’ombe alikamatiwa.

Mwenyekiti wa jumuiya hiyo, Elias Chama akiwa eneo la tukio alisema juzi jioni simba walimuua ng’ombe wa mfugaji huyo, lakini walifanikiwa kuwafukuza kabla hawajaanza kula nyama.

Chama alidai kuwa gharama ya simba kwa uwindaji wa kitalii ni Sh25 milioni, hivyo wangewindwa wangeingiza Sh175 milioni.

Mtuhumiwa anadaiwa kutoroka kwa kutumia pikipiki na kwamba, alikuwa miongoni mwa wanachama wa jumuiya hiyo waliojitokeza kugombea nafasi ya mwenyekiti na baadaye alijitoa. Madaktari wa Mifugo Wilaya ya Serengeti, Tito Kagize na Ahmed Lugelo walisema sumu hiyo ilisababisha damu kuvujia ndani ndiyo.

“Tunahisi ni sumu maana dalili zake zipo, kwanza vifo vya wanyama wengi kwa muda mfupi, chanzo cha vifo ni kimoja wamekula nyama ya ng’ombe na inaonekana walikula zaidi kitoto cha ndama, matokeo zaidi tunasubiri majibu ya mkemia maana vipimo vyote vinapelekwa huko,” alisema Dk Kagize.

Hata hivyo, msako ulioendeshwa na polisi nyumbani kwa mtuhumiwa unadaiwa kukuta ngozi ya ng’ombe iliyoraruliwa, nyama iliyokuwa imebaki na chupa moja iliyokuwa na harufu ya sumu ambayo haijajulikana.


No comments: