Sunday 9 November 2014

Simba yakumbuka shuka wakati asubuhi ishafika

http://www.hivisasa.co.tz/wp-content/uploads/2014/09/OKWI-VS-GOR-MAHIA.jpg
Emmanueli Okwi

HATIMAYE klabu ya Simba jioni ya leo imeondoa 'gundu' baada ya kuichapa Ruvu Shooting kwa bao 1-0 katika pambano la Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa ni ushindi wa kwanza katika mechi 13 ilizocheza tangu msimu uliopita.
Bao pekee lililowapa faraja wana Simba liliwekwa kimiani na Mganda Emmanuel Okwi katika dakika ya 78 akimalizia mpira uliotemwa na kipa wa Ruvu Shooting aliyepangua kiki ya Elias Maguli.
Simba ambayo ilikuwa imetoka sare mechi sita zilizopita ilikuwa ikihitaji ushindi kwa hali yoyote ili kutuliza munkari ya mashabiki na wanachama wao sambamba na kuondoa dhana kwamba 'HAIWEZI KUSHINDA' mpaka uongozi ukutane na kundi na wanachama walipachikwa jina la UKAWA.
Kwa ushindi huo Simba imefikisha jumla ya pointi 9 na kuchuku toka nafasi ya 11 hadi nafasi ya saba wakati ligi ikienda mapumziko kwa wiki kadhaa.
Bao alililofunga leo Taifa limemfanya Okwi kufikisha jumla ya mabao matatu moja nyuma ya wachezaji waongooza kwenye orodha ya vinara wa mabao wa ligi hiyo, Danny Mrandwa wa Polisi-Moro, Ame Ally 'Zungu', Didier Kavumbagu wa Azam na Rama Salim wa Coastal Union.
Katika mechi nyingine iliyochezwa uwanja wa Chamazi, JKT Ruvu wameizima Ndanda Fc ya Mtwara kwa kuichapa mabao 2-0.
Vijana wa Fred Felix Minziro waliotoka kupokea kipigo cha bao 2-1 toka Polisi Moro walipata mabao yake kupitia kwa Samuel Kamuntu na Najim Magulu na kuifanya JKT kufikisha jumla ya pointi 10 na kukwea hadi nafasi ya sita.

No comments: