Tuesday 2 December 2014

Mchakato wa kupata mwanasoka bora wa dunia wafika patamu

Mchakato wa kupata mwanasoka bora wa dunia, maarufu kama Ballon d’Or umefika pazuri, huku anayeshikilia tuzo hiyo, Cristiano Ronaldo na Lionel Messi aliyekuwa nayo kwa miaka minne pamoja na Manuel Neur wakiwamo.
Ronaldo wa Real Madrid, Messi wa Barcelona na Neur wa Bayern Munich na timu za mataifa yao – Ureno, Argentina na Ujerumani kwa mtiririko huo, wamechaguliwa kutoka kundi la wachezaji 23 lililomjumuisha Gareth Bale wa Real Madrid na Taifa la Wales. Mshindi atatangazwa Januari 12.
kipaRonaldo (29) amefunga mabao 51 katika msimu wa soka wa 2013/14 na kuwasaidia Real Madrid kutwaa ubingwa wa Ulaya. Aliwashinda Franck Ribery wa Bayern Munich na Messi katika tuzo hiyo mwaka jana.
Messi (27) ametwaa tuzo hiyo miaka minne fululizo, kuanzia 2009 hadi 2012 na amevunja rekodi ya ufungaji mabao katika Ligi Kuu ya Hispania, La Liga, na sasa anashikilia pia rekodi ya kufunga mabao mengi Ligi ya Mabingwa Ulaya, akichuana kwa karibu na Ronaldo.

Kwa upande wa Neuer (28) anakuwa kipa wa kwanza kuvuka hadi hatua ya wachezaji watatu bora wa dunia tangu raia mwenzake wa Ujerumani, Oliver Kahn kufikia hapo 2002. Neur alichangia kwa kiasi kikubwa mafanikio ya Ujerumani kwenye Kombe la Dunia na Bayern kutwaa ubingwa wa Bundesliga msimu uliopita.
Katika hatua nyingine, Kocha wa Real Madrid, Carlo Ancelotti, yule wa Timu ya Taifa ya Ujerumani aliyetwaa nayo Kombe la Dunia mwaka huu Joachim Low na Kocha wa Atletico Madrid, Diego Simeone wamevuka kuwania Kocha Bora wa Mwaka wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).

No comments: