Friday 19 December 2014

Rais wa Kenya aidhinisha sheria Mpya ya usalama


Rais Uhuru Kenyatta
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta, ameidhinisha sheria mpya ya usalama ambayo inawezesha majasusi kunasa mawasiliano kisiri au kufanya udukuzi pamoja na kuwazuia washukiwa wa ugaidi kwa mwaka mmoja kabla ya kuwafungulia mashitaka.
Kenyatta anasema kuwa sheria hiyo mpya inahitajika kwa ajili ya kukabiliana na tisho la ugaidi kutoka kwa kundi la wapiganaji wa kiisilamu la Al Shabaab.
Amesisitiza kuwa sheria hio haikiuki haki za binadamu wala kuwapokonya watu uhuru wa kujieleza.
Mnamo siku ya Alhamisi, wabunge wa serikali na wa upinzani walipigana makonde bungeni wakijadili marekebisho kwa mswada kabla ya Rais kuupitisha kuwa sheria.
Katika vurugu hizo mmoja wa wabunge wa upinzani alimmwagia maji naibu spika.
Sheria hizo mpya zilipitishwa na bunge licha ya pingamizi kubwa na vurugu kutoka kwa wabunge hao.
Vyombo vya habari vimesema baadhi ya vipengee vya sheria hio ninabana uhuru wa vyombo vya habari na hata kutishia kwenda mahakamani.
Mswada huo kabla ya kutiwa saini na kufanywa sheria,ulifanyiwa mabadiliko kadhaa katika vipengee ambavyo vilionekana na baadhi ya wabunge kama vilivyokua vikali na kwenda kinyume na katiba.
Vurugu katika bunge la Kenya wabunge walipokuwa wanajadili mswada wa sheria kali ya usalama
Polisi sasa watakuwa na jukumu la kuidhinisha taarifa au picha za uchunguzi wa maswala ya usalama na hasa kuhusiana na ugaidi.
Polisi pia ndio watapaswa kuidhinisha picha za waathiriwa wa ugaidi kabla ya kuchapishwa au kuonyeshwa katika vyombo vya habari.
Vyombo vya habaro vinasema haya yanakwenda kinyume na uhueu wa vyombo vya habari.
Adhabu itakayotolewa kwa watakaokiuka sheria hii ni hadi faini ya shilingi milioni tano au dola elfu sitini ama kufungwa jela kwa zaidi ya miaka mitatu.

No comments: