Friday 27 February 2015

Siri Nzito zzaibuka kuhusu viungo vya albino

Kila kiungo kimoja cha ‘albino’, huuzwa kwa bei kubwa, hali inayotajwa kuwa kiini cha kukithiri kwa mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi, mahakama mkoani Geita ilielezwa jana.Ingawa bei ya viungo vya albino ilitajwa jana mahakamani, lakini hatuwezi kutaja thamani hiyo ili kuwalinda watu wenye ulemavu wa ngozi.
Akitoa ushahidi katika kesi namba 43/2009 ya mauaji ya albino, Zawadi Magimbu, mkazi wa Kijiji cha Nyamaruru wilayani Geita, shahidi wa 12 ambaye ni polisi wa upelelezi kutoka Makao Makuu ya Polisi, Dar es Salaam aliibua mambo lukuki ya ajabu yanayofanywa na wauaji wa albino.
Mambo hayo ni pamoja na thamani ya fedha wanazolipwa watu kwa kila kiungo kimoja cha albino kiasi cha (tunahifadhi)katika Kanda ya Ziwa, huku viungo hivyo pia vikitofautishwa ubora kwa kupimwa na redio, wembe na Sh1 ya zamani.
Washtakiwa katika kesi hiyo ni Masaru Kahindi, Ndahanya Lumola, Nassoro Charles na Singu Siantem. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Machi 5 itakapotolewa hukumu.
Akitoa ushahidi mbele ya Jaji Joacqiune Demello, shahidi huyo (jina linahifadhiwa), alidai upelelezi wa polisi ulibaini kuwa wakati wa mauaji ya mwaka 2008, watuhumiwa walikuwa wanashawishiwa kulipwa kiasi kikubwa kwa kila kiungo kimoja cha albino.
“Nilitoka Dar es Salaam kuja Mkoa wa Shinyanga kufanya upelelezi wa mauaji ya albino. Nikiwa Shinyanga, tulipata taarifa kutoka kwa msiri wetu aliyetueleza kuna watu wanafanya biashara ya viungo vya albino,” alidai shahidi huyo.
Alidai baada ya kupata taarifa hizo, waliamua kuweka mtego ili kuwakamata watu hao waliokuwa wakijishughulisha na biashara hiyo.
“Tulitafuta albino wawili kwa ajili ya mtego na kafanikiwa kuwakamata watu wawili, ambao ni Robert Magoma na Ndahanya Lumola waliokuwa wakijishughulisha na biashara hiyo,” alidai shahidi huyo.
“Katika uchunguzi wetu, tuligundua kuwa kuna mganga aliyetajwa kwa jina la Gerald Mazuri, mkazi wa Kijiji cha Kakoyoyo, Kata ya Ushirombo, Wilaya ya Bukombe kuwa anafanya biashara hiyo na Wazungu kutoka Wilaya ya Geita (hawakutajwa).
Alidai kuwa wembe, redio na shilingi hutumika kama vipimo vya kujua ubora wa viungo vya albino.
“Niliendelea kuwadadisi, wakasema walipeleka mifupa hiyo kwa Mganga wa Jadi, Mussa Ally wa mjini Katoro, mkoani Geita ikapimwa kwa kutumia wembe, redio inayozungumza na Sh1 ya zamani,” alidai shahidi huyo na anamnukuu mmoja wa washtakiwa:
“Ukichukua wembe ukauweka kwenye mfupa wa albino na kunasa, basi mfupa huo ni dili, kinyume chake hauna ubora. Pia, ukichukua Sh1 ukaiweka kwenye mfupa na kunasa, nao ni bora na redio inayozungumza ukiisogeza kwenye mfupa huo na kuzima, ujue kiungo hicho ni dili.”
Desemba 27 mwaka jana, mtoto Pendo Emmanuel (4), alitekwa na watu wasiojulikana katika Kijiji cha Ndami, Wilaya ya Kwimba.
Februari 15, mwaka huu, mtoto Yohana Bahati (1), alitekwa kabla ya kuokotwa akiwa amekufa na miguu na mikono yake kukatwa.
Hivi karibuni, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani, ilipiga marufuku waganga wa jadi kupiga ramli.

No comments: