Monday 22 June 2015

Vurugu za ibuka katika vituo vya kujiandikisha kupiga kura

Mbunge wa Arusha Mjini, Godbles Lema.MILIO ya risasi ilisikika katika vituo vya uandikishaji kura katika kata ya Sokoni One jijini hapa, baada ya kuibuka kwa vurugu zilizohusisha vijana wa Chadema na wenzao wa CCM, chanzo kikitajwa madai ya kuwepo kwa watu ambao sio wakazi wa eneo hilo kutaka kujiandikisha.
Vurugu hizo zilisababisha takribani watu 15 kukamatwa akiwemo Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, Godbless Lema (Chadema) ambaye hata hivyo baadaye aliachiwa huru. Alishikiliwa kuanzia saa 1:30 usiku hadi saa 4:00 usiku juzi.
Patashika hiyo ilichukua zaidi ya saa moja, kwani baadhi ya polisi waliokuwa na silaha za moto aina ya bastola walifyatua risasi hewani kwa lengo la kutawanya vurugu hizo, lakini hali ilikuwa mbaya zaidi hadi polisi walipoongezwa na kufanikiwa kutuliza ghasia hizo.
Wakati hayo yanatokea Lema alisisitiza kuwa kamwe hawezi kukubali kutohamasisha wananchi kwenda kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapigakura licha ya kudai kuwa, kundi la vijana wanaosadikiwa kuwa wa CCM wamempiga mawe sambamba na watu wengine waliojitokeza kujiandikisha katika kata mbalimbali.

Hata hivyo, upande wa vijana wa CCM, umedai wenzao wa Chadema ndio chanzo cha vurugu, kwani wameonekana wakisambaza makundi ya vijana wasiostahili kuandikisha katika vituo mbalimbali.
Lema ajitetea Akizungumzia kukamatwa kwake na polisi wa kata ya Osunyai kutokana na vurugu zilioibuka, alidai alikuwa akitoa taarifa za uongezwaji wa mashine za BVR kwa wananchi na kuwapa moyo kuwa watulivu wakati wa uandikishwaji sambamba na kutunza vitambulisho hivyo kwa ajili ya kupiga kura mwaka huu katika uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani.
Alisema wakati akiendelea kuwapa moyo wananchi na kusema Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imeongeza mashine za BVR, ghafla aliona vijana anaodai wamekodishwa kufanya vurugu kwenye vituo mbalimbali vya kujindikisha na ndipo alitoa taarifa Polisi, lakini badala ya kukamata vijana hao alikamatwa yeye na vijana wengine na kuweka mahabusu.
NEC iliruhusu uandikishaji kuendelea hadi saa mbili usiku kutokana na wingi wa watu wanaostahili kuandikishwa. Hata hivyo mmoja wa wafuasi wa CCM aliyejitambulisha kwa jina la Abdi Marijani maarufu kwa jina la ‘`Mutu’ alisema Chadema wamekuwa wakileta watu ambao sio wakazi Jiji la Arusha kutaka kujiandikisha hali iliyopingwa na vijana hao.
Mutu alisema CCM ilikuwa imepewa taarifa juu ya njama za Chadema za uchomekeaji watu katika kila kata na chama kikaweka vijana imara katika kila kituo wakiwa na mabalozi ambao ndio wenye jukumu la kujua mkazi wa eneo husika.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Lema alisema juzi akiwa kata ya Osunyai alishangaa kuona kundi la vijana wakiwa kwenye gari aina ya Toyota Land Cruiser lenye namba za usajili T 122 ATR ambalo alidai wakati mwingine gari hilo lilibadilishwa namba na kusomeka T 122 ABR wakishuka ghafla na kuanza kumpiga mawe na kuwapiga vijana wengine 25 ambao walikuwa katika kituo hicho.
Alisema wakati tukio hilo likitokea alitoa taarifa kwa Mkuu wa Upelelezi wa wilaya OC/CID, Faustine Mwafele ili kuwaelezea tukio hilo, lakini polisi walifika eneo la tukio badala ya kuwakamata vijana hao walimkamata yeye na vijana waliokuwepo kisha kuwaweka chini ya ulinzi.
Alisema inaonekana kundi hilo linaonekana lipo juu ya sheria watu wanafanya fujo za waziwazi, huku mbunge akigeuziwa `na kusulubiwa.
Alisema kwa kuwa yeye ni mbunge, hawezi kuacha kuhamasisha wananchi wake kujiandikisha badala yake chama chao na viongozi wa chama wataendelea kuhamasisha watu kujitokeza kujiandikisha sambamba na kuhamasisha watu wasikate tamaa katika kujiandikisha kwa sababu ni wajibu wao wa kisheria, kisiasa na kidemokrasia.
Aliongeza kuwa udhalilishwaji sasa umefika mwisho, hivyo alitoa rai kwa vijana wa chama hicho kuchukua hatua ya kuwalinda viongozi wao, kulinda demokrasia na mali zao.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas hakupatikana kuzungumzia tukio hilo, licha ya kutafutwa kupitia simu yake ya mkono ikiwa ni pamoja na kutumiwa ujumbe mfupi wa maandishi.
Wasemavyo CCM Akizungumzia hilo, Katibu wa CCM wa Wilaya ya Arusha, Feruz Banno alisema vurugu zilianzishwa na vijana wa Chadema kwa kuwapiga vijana wa CCM na kupiga risasi hewani hovyo bila ya sababu za msingi.
Banno alisema dola Arusha inapaswa kuwa makini, kwani hali inaweza kuwa mbaya zaidi iwapo hilo halitadhibitiwa na kuwafanya watu wengine kushindwa kwenda kujiandikisha kwa kuogopa vurugu.
Alisema kutokana na vurugu zinazofanywa kwenye baadhi ya vituo vya kujiandisha na baadhi ya viongozi wa Chadema ili kudhibiti wazee na akinamama wanaokwenda kujiandikisha kwenye vituo hivyo.
Alisema kwa sasa uandikishaji unafanyika katika kata za Terati, Murieti, Olusunyai, Moshono, Sinoni na Sokoni One, lakini baadhi ya vijana wa chama hicho wamekuwa wakisafirishwa kwa magari kutoka kata tofauti na hizo na kupelekwa eneo hilo kwa ajili ya kujiandikisha .
Ulinzi Kwa upande wake Marijani, alisema kutokana na udhibiti uliowekwa na makamanda wa CCM vituo vya kupigia kura wamebaini kuwa viongozi wa Chadema na vijana wao wamekuwa wakileta vurugu katika kila kituo ili zoezi hilo lisiweze kufanikiwa.
“Tumeweka ulinzi kila kituo na hiyo itakuwa ikifanyika katika kata zote za Jiji la Arusha kwani hiyo itasaidia kupata wakazi halisi wa eneo husika na sio mamluki,” alisema Mutu.

No comments: