Friday 24 July 2015

SZCZESNY kuondoka Arsenal


huyooo Roma....
huyooo Roma….
Golikipa wa Arsenal, Wojciech Szczesny, 25, anaondoka klabuni hapo kujiunga na Roma kwa mkataba wa mkopo wa mwaka mmoja.
Szczesny aliruhusiwa na Arsenal kufanya mazungumzo na Roma juu ya maslahi yake, kwani tayari wanaye Petr Cech aliyesajiliwa kutoka Chelsea na David Ospina aliyempoka Szczesny namba yake katikati ya msimu uliopita.

Kusajiliwa kwa Cech kumemaanisha kwamba Szczesny anakuwa chaguo la tatu wakati anataka kupata muda zaidi wa kusakata soka katika umri wake wa miaka 25. Roma wamekuwa wakitaka kumsajili moja kwa moja lakini Arsene Wenger hataki kuachana na Mpolandi huyo.
Roma wanatarajiwa kuwalipa Arsenal pauni 250,000 za kuanzia kabla ya kuweka sawa ada kamili ya uhamisho huo.
Arsenal wameeleza kutaka kumsajili kiungo mkabaji wa Barcelona, Sergi Samper, 20, lakini mkataba wake unataka klabu inayomtaka itoe pauni milioni 8.5. Porto, Everton na Stoke wamemuuliza mchezaji huyo pia,
Wenger alijaribu kumsajili Samper 2011 alipomleta Emirates, Hector Bellerin.
Katika tukio jingine, kiungo mkongwe wa Arsenal aliyesajiliwa kama mchezaji huru, akijiunga na Arsenal kwa mara ya pili, Mathieu Flamini anatarajiwa kuondoka Emirates na kujiunga na Galatasaray nchini Uturuki.
Inasemekana kwamba Galatasaray wamewalipa Arsenal pauni milioni nne kwa ajili ya Flamini (31) na sasa ataungana na mchezaji mwenzake aliyekuwa Arsenal, Lukas Podolski.
Flamini alijiunga na Arsenal kwa mara ya pili akitoka AC Milan 2013, baada ya kuwa amefanya kazi na Wenger tangu 2004 hadi 2008 akiwa na kiwango kikubwa tofauti na sasa.

No comments: