Thursday 26 November 2015

Bunge la Uingereza la jadili kuhairishwa kwa uchaguzi Zanzibar

http://mtanzania.co.tz/wp-content/uploads/2015/11/mtz14.jpgHALI ya kisiasa na kufutwa kwa uchaguzi wa urais pamoja na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar hatimaye imetua na kujadiliwa katika Bunge la mabwanyenye la nchini Uingereza.
Uamuzi huo umekuja siku moja baada ya wapinzani wawili wa kisiasa visiwani humo, Rais Dk. Ali Mohamed Shein na Makamu wake wa Kwanza ambaye pia alikuwa mgombea wa urais kupitia CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, kuendelea na vikao vya siri vinavyoshirikisha marais wastaafu wa Zanzibar.
Sakata hilo liliibuka jana nchini Uingereza katika kikao cha Bunge ambapo mbunge Lord Steel wa Aikwood kutoka Chama cha Liberal Democrat, alitaka kujua tathmini ya Serikali ya Uingereza kuhusu uchaguzi nchini Tanzania, hasa ule wa Zanzibar na kilichoelezwa kwa Serikali ya Tanzania au Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola kuhusu uchaguzi huo.

Kutokana na swali hilo, Waziri wa Nchi, Baroness Anelay wa St. Johns, alisema kuwa pamoja na kuwapo matatizo kadhaa, uchaguzi wa Tanzania ulifanyika kwa amani na uliendeshwa vyema.
Alisema kutokana na hali hiyo, Serikali ya Uingereza ilitoa pongezi kwa Rais Dk. John Magufuli kutokana na ushindi wake alioupata katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 25, mwaka huu.
“Tulitoa pongezi zetu kwa Rais Magufuli kufuatia ushindi wake. Hata hivyo, tulisikitishwa na uamuzi wa kufuta uchaguzi wa urais na uwakilishi Zanzibar.
“Kwa nyakati tofauti tulieleza masikitiko yetu kwa Serikali ya Tanzania kuhusu hilo, ikiwamo katika ngazi za juu na hivi karibuni kabisa ilikuwa wiki iliyopita wakati wa mkutano baina ya Balozi wa Tanzania mjini London na Waziri Mdogo wa Nchi kwa Masuala ya Kigeni na Jumuiya ya Madola, Mheshimiwa Mbunge wa Rochford na Southend East, James Duddridge,” alisema Anelay.
Pamoja na suala hilo la kujadiliwa kwa uchaguzi wa Zanzibar nchini humo, lakini bado kumekuwa na mazungumzo kadhaa ya kutafuta mwafaka wa suala hilo ambapo CUF kimekuwa kikitaka matokeo yatangazwe na mshindi aapishwe, huku upande wa CCM, ukieleza kuwa mazungumzo yanayoendelea hayazuii kufanyika kwa uchaguzi mwingine.
Mazungumzo hayo ya kutafuta mwafaka wa mgogoro wa Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar, yameendelea kufanyika juzi  Ikulu mjini Unguja.
Kikao hicho cha tatu kilikuwa chini ya Dk. Shein, huku akimshirikisha Maalim Seif.
Taarifa kutoka Ikulu ya Zanzibar zilieleza kwamba pamoja na kikao hicho kuwakutanisha mahasimu hao wa kisiasa, pia kimehudhuriwa na wajumbe ambao ni marais wastaafu wa Zanzibar, Dk. Salmin Amour, Amani Abeid Karume, Alhaji Ali Hassan Mwinyi na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi.
Matokeo ya mazungumzo hayo yamekuwa yakisubiriwa kwa hamu kubwa na wananchi baada ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), kupitia Mwenyekiti wake, Jecha Salim Jecha, kutoa tamko la kufutwa kwa uchaguzi huo, Oktoba 28, mwaka huu jambo ambalo liliibua mgogoro wa kikatiba.
Novemba 9, mwaka huu, mawaziri sita wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa kutoka CUF walijiuzulu kutokana na msuguano huo wa kisiasa visiwani humo.
Mgogoro wa kisiasa Zanzibar umekuwa ukichukua sura tofauti, ambapo wiki iliyopita Wazanzibari wanaoishi nchini Uingereza walifanya maandamano na kuitaka nchi hiyo iingilie kati na kutoa shinikizo kwa Serikali ya Tanzania ili kuhakikisha mshindi wa uchaguzi wa rais wa Zanzibar anatangazwa na kuapishwa.
Wazanzibari hao walifikia uamuzi huo kutokana na hatua ya Mwenyekiti wa ZEC, Jecha, kutangaza kufuta matokeo ya uchaguzi, huku akitoa sababu tisa ikiwamo uchaguzi huo kutokuwa huru na haki.
Maandamano hayo yaliishia katika Mtaa wa Downing zilipo ofisi za Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron na kukabidhi barua yao.
Mbali na Uingereza, Wazanzibari wanaoishi nchini Marekani nao pia waliandamana hadi Ikulu ya nchi hiyo, ikiwa ni juhudi za kutafuta uingiliaji kati wa kimataifa ili kuupatia suluhisho mzozo huo.
Akizungumza na waandishi wa habari juzi mbele ya Ikulu hiyo, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazanzibari Waishio Marekani (ZADIA) iliyoandaa maandamano hayo, Omar Haji Ali, alisema uamuzi wao huo ni katika juhudi za kutafuta uingiliaji kati wa kimataifa katika kuukwamua mgando wa kisiasa visiwani Zanzibar.

No comments: