Monday 23 November 2015

Wapinzani wachukua dola Argentina

Macri
Macri alikuwa ameshindwa kwenye duru ya kwanza

Mgombea wa chama cha upinzani cha Conservative Mauricio Macri amethibitishwa kuwa mshindi wa uchaguzi wa urais Argentina, huku mgombea wa chama tawala akikubali kushindwa.
Baada ya karibu kura zote kuhesabiwa, Bw Macri alikuwa na 52% akilinganishwa na Daniel Scioli aliyepata 48%.
Shangwe na vigelegele vilitanda katika makao makuu ya kampeni ya Bw Macri baada ya kura za maoni runingani kuonyesha alikuwa ameshinda.
Bw Macri, meya wa zamani wa Buenos Aires, alikuwa ameshindwa na Scioli, ambaye ni gavana wa mkoa wa Buenos Aires, kwenye duru ya kwanza ya uchaguzi Oktoba.
Lakini wote wawili hawakuweza kushinda moja kwa moja na duru ya pili ikaandaliwa, mara ya kwanza kwa uchaguzi kuingia duru ya pili katika historia ya Argentina.
Ushindi wa Bw Macri ndio wa kwanza katika zaidi ya mwongo mmoja kwa upinzani wenye kuegemea siasa za mrengo wa kati kulia.

Aliingia kwenye uchaguzi huo wa Jumapili akiwa mbele kwa kura za maoni na alikuwa ameahidi kusisimua uwekezaji na kukabili changamoto za kiuchumi, uhalifu na ufisadi.
Bw Macri ni mwana wa mmoja wa watu tajiri zaidi Argentina na alifanya kazi kwa muda mrefu kama mwanabiashara kabla ya kujitosa katika siasa.
Bw Scioli ni mshirika wa karibu wa Rais anayeondoka Cristina Fernandez de Kirchner
 
Bw Scioli, ambaye ni mwandani mkuu wa Rais anayeondoka Cristina Fernandez de Kirchner, alikuwa ametarajiwa kushinda duru ya kwanza iliyofanyika Oktoba kwa kura nyingi lakini hilo halikuwa.

No comments: