Saturday 12 December 2015

Mtoto wa Gaddafi aachiwa huru

HannibalHannibal amekuwa kwenye kizuizi cha nyumbani Oman tangu 2012
Mwana wa kiume wa aliyekuwa kiongozi wa Libya Muammar Gaddafi, Hannibal, ameachiliwa huru baada ya kutekwa nyara kwa muda na kundi la wapiganaji, duru za kiusalama zinasema.
Kwenye video iliyoonyeshwa kwenye runinga ya Lebanon, mfanyabiashara huyo alionekana akiitisha habari zaidi kuhusu kutoweka kwa mhubiri mashuhuri wa dhehebu la Washia nchini Lebanon Musa al-Sadr. Al-Sadra alitoweka mwaka 1978. Alionekana kwenye video hiyo akiwa amejeruhiwa machoni.

Aliachiliwa huru katika mji wa Baalbek na kupelekwa mjini Beirut, polisi waliambia shirika la habari la AP.
Hannibal, 40, alipatiwa hifadhi na Oman mwaka 2012.
Babake aliondolewa mamlakani kupitia mapinduzi yaliyotokana na maasi 2011.
Al-Sadr, mmoja wa viongozi mashuhuri wa Washia wa karne ya 20, alitoweka pamoja na watu wengine wawili akiwa ziarani Libya mwaka 1978.
Muammar Gaddafi alikanusha kuhusika, lakini wengi wanashuku ndiye aliyehusika.
Tukio hilo liliathiri uhusiano kati ya Libya na Lebanon.
Haijabainika Hannibal alikuwa nchini Lebanon kwa muda gani.
Alikuwa amewekwa kwenye kizuizi cha nyumbani nchini Oman pamoja na dadake Ayesha na mamake Safiya.

No comments: