Friday 5 February 2016

India: Wengine 'waliomvua nguo' Mtanzania mbaroni

GariGari la wanafunzi hao liliteketezwa
Washukiwa zaidi wamekamatwa na maafisa wa polisi nchini India kuhusiana na kisa ambapo mwanafunzi Mtanzania alipigwa na kuvuliwa nguo mjini Bangalore.
Washukiwa wengine wanne wamekamatwa na kufikisha tisa, jumla ya washukiwa wanaozuiliwa na polisi.
Maafisa watatu wa polisi pia wamesimamishwa kazi, wakisubiri kufanyiwa uchunguzi.
Watatu hao wanatuhumiwa kukataa kupokea malalamiko kuhusu kushambuliwa kwa mwanafunzi huyo wa kike wa umri wa miaka 21 pamoja na wenzake wa tatu.
Balozi wa Tanzania nchini India John WH Kijazi anatarajiwa kukutana na waziri wa mambo ya ndani ya jimbo la Karnataka.

Baadaye, atakutana na wanafunzi waliodhalilishwa karibu na chuo chao.
Maafisa wawili kutoka afisi ya wizara ya mambo ya nje ya India wataandamana na balozi huyo.
Kisa cha kushambuliwa kwa wanafunzi hao kimeshutumiwa vikali na serikali ya Tanzania ambayo imeitaka India kuhakikisha usalama wa wanafunzi wanaoishi na kusomea humo.
Watanzania mtandaoni pia wamekuwa wakishutumu kisa hicho na kuitaka serikali kuchukua hatua.
Tangu kutokea kwa kisa hicho, wanafunzi wengi kutoka Tanzania wamekuwa wakihofia usalama wao.

No comments: