Saturday 2 April 2016

Zuma akubali makosa kuhusu ukarabati Nkandla

Zuma
Mahakama ya Kikatiba ilimtaka Zuma alipe gharama ya ukarabati

Rais wa Afrika Kusini Jacob Zuma amekubali uamuzi wa Mahakama ya Kikatiba uliompata na hatia kuhusiana na ukarabati uliofanywa katika makao yake ya kibinafsi eneo la Nkandla.
Akihutubia taifa hilo moja kwa moja kupitia runinga, Bw Zuma amesifu mahakama hiyo na kusema imedhihirisha kuwepo kwa uhuru wa mahakama nchini humo.
Amesema uamuzi wa mahakama hiyo ni wa kihistoria kuhusu uamuzi wa mkaguzi wa hesabu za umma aliyewasilisha kesi dhidi yake mahakamani.
"Mahakama imeamua kwamba uamuzi wa mkaguzi wa hesabu za umma ni wa mwisho na anayetaka kubadili hilo lazima apitie kwa mahakama," amesema Bw Zuma.
Kiongozi huyo amesema atakubali kulipia ukarabati uliofanyiwa makao hayo ya Nkandla kama ilivyoamua mahakama.

"Nimekuwa nikisisitiza kwamba niko tayari kulipia ukarabati usiohusiana na usalama katika mahakama yangu, taasisi rasmi ikifanya hesabu hiyo na kutoa uamuzi," amesema.
Bw Zuma amesema pia kwamba anakubali kwamba hatua yake ya kukosa kutii uamuzi wa mkaguzi wa hesabu za umma ni makosa na ukiukaji wa katiba.
Hata hivyo amesisitiza kwamba hakufanya hivyo makusudi.
"Awali, nilifuata njia tofauti ambayo ni sahihi kisheria wakati huo, lakini baadaye imebainishwa kuwa kinyume cha katiba. Kama Mahakama ya Kikatiba ilivyosema, nilifuata njia tofauti nikifuata uamuzi wa Mahakama ya Juu ya Western Cape. Uamuzi huu baadaye ulibatilishwa baada ya rufaa na mara moja nilianza kufuata uamuzi wa Mahakama ya Rufaa," amesema.
"Nia yangu haikuwa kutaka kujinufaisha kupitia ufisadi au kutumia mali ya umma kujifaidi au kufaidi familia yangu. Hivyo, nimeamua kulipia gharama ya vitu vinavyotakikana utathmini ukifanywa."
Amesema kuna mafunzo ya maafisa wa serikali kujifunza kwa ajili ya siku za usoni.
Ameeleza kuwa mradi huo wa Nkandla umefichua udhaifu wa mfumo wa ununuzi wa mali ya umma. Amekiri kwamba gharama ya ukarabati wa makao yake iliongezwa sana jambo ambalo halikufaa kufanyika.

No comments: