Tuesday 4 April 2017

Shahidi wa kesi ya scorpion anusurika kutupwa jela

Mkazi wa Buguruni jijini hapa, Deus Johakim Magosa (45) ambaye ni shahidi wa nane upande wa Jamhuri katika kesi namba 303 ya mwaka 2016 ya kumjeruhi, kumtoboa macho na kumfanyia unyang’anyi wa kutumia silaha, Saidi Mrisho inayomkabili Salum Njwete ‘Scorpion’ katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala jijini, leo alinusurika kutupwa lupango baada ya Wakili Mwandamizi wa Serikali, Nassoro Katuga kumtuhumu kutoa ushahidi wa uongo.
Wakili Katuga alimtuhumu shahidi huyo  kutokana na kutoa majibu tofauti wakati akimuongoza kutoa ushahidi wake na maelezo aliyoyatoa awali Kituo cha Polisi cha Buguruni.
Awali shahidi huyo alisema mahakamani hapo kuwa hakuwahi kusikia popote kuwa Scorpion amehusishwa katika tukio la kumshambulia Said, lakini baadaye alipobanwa alisema ni kweli alisikia tetesi hizo kuwa mtuhumiwa huyo ndiye aliyefanya tukio hilo. Pamoja na mambo mengine aliyomhoji na kumbaini kuwa anatoa ushahidi wa uongo wakili Katuga
alipomgeukia hakimu aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo, Flora Haule  na kumwambia shahidi anazidi kuidanganya mahakama hiyo na kuitaka mahakama hiyo imchukulie hatua kwa mujibu wa kifungu cha 164 cha ushahidi hapa nchini (Tanzania Evidence Act).
Shahidi huyo alionekana kuwa katika wakati mgumu baada ya wakili huyo kuwaita askari polisi na kuwataka wakae tayari kumchukua shahidi huyo.
Hata hivyo kutokana na ufinyu wa muda hakimu Flora aliahirisha kesi hiyo mpaka Aprili 18 mwaka huu na kumuacha shahidi huyo aondoke na kumtaka kufika tena mahakamani hapo tarehe iliyopangwa bila kukosa ambapo Scorpion naye alirudishwa mahabusu mpaka tarehe hiyo.
Mwandishi wetu alizungumza na mmoja wa wanasheria mahakamani hapo kuhusu ushahidi wa uongo ambapo, mwanasheria huyo alisema unapobainika kutoa ushahidi wa uongo ukiwa ndani ya kiapo unaweza kufungwa jela kati ya miezi sita mpaka mwaka mmoja.

No comments: