Wednesday 15 November 2017

Jeshi la Zimbabwe la kanusha kufanya mapinduzi

Jeshi la Zimbabwe limekanusha madai kwamba mapinduzi ya kijeshi yamefanyika kuiondoa serekali, na kudai kwamba rais Robert Mugabe na familia yake wapo salama.Katika taarifa iliyotolewa na jeshi kupitia televisheni ya taifa, imeelezwa kwamba jeshi linalenga wahalifu wanaosababisha shida za kijamii na kiuchumi na kuwafikisha mbele ya sheria.


Taarifa hiyo imetolewa baada ya mashuhuda kusema wamesikia takriban milipuko mitatu pamoja na milio ya risasi katika mji mkuu wa Harare, usiku wa kuamkia Jumatano.
Inaelezwa pia na mashuhuda magari ya jeshi na wanajeshi walikuwa katika mitaa mapema Jumatano hii saa kadhaa baada ya wanajeshi kushikilia chombo cha utangazaji cha serekali cha ZBC.
Wakazi wamesema kwamba tofauti na kuwepo kwa taarifa ya habari ya saa tano usiku, ZBC ilicheza muziki bila taarifa yoyote.
Msemaji wa ubalozi wa Marekani mjini Harare, alinukuliwa akisema kwamba mitaa ya Harare ilionekana kuwa tulivu usiku wa kuamkia leo, na hakuthibitisha kuona magari ya kijeshi. Msemaji huyo pia amesema hana taarifa ya milipuko yoyote kutokea kama ilivyoelezwa na baadhi ya wakazi wa Harare.
Hapo jana Jumanne, chama tawala nchini Zimbabwe ZANU-PF kilimshutumu mkuu wa majeshi kwa vitendo vya uhaini baada ya kutishia kuingilia kati mgogoro wa kisiasa wa nchi hiyo.
Taarifa ya ZANU-PF ilitolewa katikati ya wasiwasi uliotanda kwamba jeshi limechukuwa hatua ya kuchukuwa madaraka na kumuondoa rais wa muda mrefu wa Zimbabwe, Robert Mugabe.
Mashuhuda waliripoti kuona vifaru na maafisa wa jeshi wakiwa mitaani na kelekea nje ya mji licha ya Harare kuwa tulivu. Balozi za nchi mbalimbali nchini humo hazikutoa tahadhari kwa raia wake walioko nchini Zimbabwe kwa sasa.
Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Marekani pia alinukuliwa akisema kwamba wanataarifa hizo na wanaendelea kufanya uangalizi.
Hali ya wasiwasi ya sasa ilizuka juma lililopita wakati rais Robert Mugabe alipomfukuza naibu wake Emmerson Mnangagwa na kumshutumu kwa kutomti na kupanga kutwaa madaraka.

No comments: